diamond alazwa wema roho juu

Rais wa Wasafi Bongo, Naseeb Abdul ‘Diamond’ ni mgonjwa, aliyekuwa mpenzi wake wa zamani, Wema Isaac Sepetu amezipata taarifa hizo na kumtumia sms nzito ‘zilipendwa’ wake huyo na kumuombea apate nafuu.
Chanzo chetu cha habari kimesema kuwa Diamond alilazwa katika Hospital ya Al-Ijumaa iliyopo kati ya Mitaa ya Sikukuu na Mafia jijini Dar es Salaam, Machi 7, mwaka huu, baada ya kupimwa na kugundulika kuwa na malaria.
Staa huyo alilazwa kwa mapumziko kutwa nzima hadi saa 2 usiku aliporuhusiwa baada ya kuonekana hali yake inaendelea vizuri.
Taarifa za kuumwa kwa Diamond zilizagaa sehemu mbalimbali hasa katika mitandao ya kijamii, ambapo ndugu na marafiki zake walifika hospitalini hapo kumpa pole.
Baada ya kupata taarifa hizo, paparazi wetu alimtafuta Diamond kwa simu yake ya mkononi ambapo alikiri kuumwa na kusema kuwa ni kutokana na shoo anazozifanya.
“Kaka ni uchovu tu wala hakuna kingine,” alisema Diamond kwa kifupi.
Risasi Jumamosi pia lilipata habari kuwa kulikuwa na mawasiliano kati ya Wema ambaye ni mnyange wa Tanzania mwaka 2006 na Diamond.
Inadaiwa kuwa Wema amemtumia sms nzito staa huyo anayetamba na kibao cha Mawazo ili kumliwaza kutokana na kuumwa.
Hata hivyo, gazeti hili lilipowasiliana na Wema alikuwa na haya ya kusema:
“Kweli nimepata taarifa za kuumwa kwa Diamond, ila nimemtumia ujumbe wa kawaida tu, siyo mzito kivile kama mlivyoambiwa, ni wa kawaida tu,” alisema.
Aidha, Wema alisema kuwa alishindwa kwenda kumuona Diamond baada ya kutopata fursa ya kufanya hivyo, ingawa  alisema kuwa aliumia kusikia kuwa amelazwa.

Comments